Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Mhe. Ummy Mwalimu amepiga marufuku magari ya kubeba wagonjwa (Ambulance ) kubeba watu au kitu chochote tofauti na wagonjwa na akawaagiza Waganga wakuu wa Mikoa na Wilaya kote nchini, kusimamia matumizi ya magari hayo na kuhakikisha yanatumika kwa matumizi yaliyokusudiwa kwa mujibu wa mwongozo.
Waziri Ummy ametoa agizo hilo Julai 12, 2018 katika uzinduzi wa Mradi wa TUWATUMIE wenye lengo la kuunganisha jamii hasa zile zilizo mbali na vituo vya tiba, ambao umezinduliwa katika Wilaya ya Itilima Mkoani Simiyu, kuunganisha jamii zinazoishi maeneo magumu kufikiwa na mfumo wa Huduma za Afya ambao umelenga kupunguza vifo vya mama na Mtoto mkoani SIMIYU.
“Nimesikitishwa sana na kitendo cha gari la kubebea wagonjwa la Halmashauri ya Mji wa Tarime mkoani Mara kubeba dawa za kulevya, ninakemea jambo hili kwa nguvu zangu zote na ninawataka waganga wakuu wa mikoa na wilaya kote nchini kusimamia matumizi ya magari ya kubebea wagonjwa “ alisema Waziri Ummy Mwalimu
“ Ni marufuku gari la kubebea wagonjwa kubeba kitu tofauti na mgonjwa, yeyote ambaye tumemkabidhi gari la kubebea wagonjwa tutamchukulia hatua kali pale ambapo atakiuka mwongozo wa matumizi ya magari ya kubebea wagonjwa, nalipongeza sana jeshi la Polisi kwa kuchukua hatua na ninamtaka Mkurugenzi wa Halmashauri husika kuwasimamisha kazi mara moja dereva na wote waliohusika na gari hilo kubeba mirungi” alisisitiza.
Akizundua mradi wa TUWATUMIE Wahudumu wa Afya Ngazi ya Jamii, Waziri Ummy amewashukuru wafadhili wa mradi huu Amref Health Africa Tanzania chini ya Ufadhili wa Serikali ya Ireland kupitia Shirika la Irish aid ambao utatekelezwa kwa kushirikiana na Benjamin Mkapa Foundation na Halmashauri za Itilima na Misungwi(Mwanza) ukiwa na lengo la kupunguza vifo vya mama na Mtoto.
Katika hatua nyingine Waziri Ummy amezitaka halmashauri zote nchini kuhakikisha zinaajiri Wahudumu wa Afya ngazi ya Jamii kutoka katika Halmashauri au wilaya husika na si vinginevyo.
Mbunge wa Itilima Mhe. Njalu Silanga ameomba Zahanati ya Lagangabili ipandishe hadhi kuwa kituo cha afya kusogeza huduma kwa wananchi, jambo ambalo limefafanuliwa na Mhe.Waziri kuwa zahanati hiyo haitapandishwa hadhi mpaka itakapojengewa miundombinu muhimu na akaahidi kutafuta shilingi milioni 400 kwa kushirikiana na wadau, ili kuwezesha ujenzi wa wodi ya wazazi, mama na mtoto na jengo la upasuaji.
Naye Mwakilishi wa Mkuu wa Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mkuu wa Wilaya ya Bariadi, Mhe. Festo Kiswaga amesema viongozi wa Mkoa wa Simiyu wanaunga mkono juhudi za Serikali na wadau mbalimbali katika kuboresha sekta ya Afya nchini, na kumhakikishia Waziri Ummy kuwa fedha yoyote itakayotolewa katika Mkoa huo itasimamiwa ipasavyo na kuleta matokeo chanya.
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Amref Dkt Aisa Muya amesema mradi huo utasaidia kuunganisha wananchi walio mbali na vituo vya tiba kupunguza vifo vya mama na mtoto chini ya miaka mitano, kutoa huduma za awali kwa jamii, kutoa elimu kuhusu njia bora za kuepukana na magonjwa, kutoa elimu kuhusu ukatili wa kijinsia na kukusanya takwimu mbalimbali za afya ya jamii vijijini.
Akizungumza kwa niaba ya wahudumu wa afya ngazi ya jamii Nkwimba Edward amesema wahudumu hao wako tayari kuhudumia jamii kwa kutoa elimu kuhusu mambo mbalimbali ya afya na akaomba Serikali na wadau waone namna ya kuwawezesha kupata usafiri wa kuwafikia wananchi.
Mradi huu utatekelezwa katika kipindi cha miaka miwili katika Wilaya mbili ambazo ni Wilaya ya Itilima inayotarajia kuwa na wahudumu wa afya ngazi ya jamii 102 na Wilaya ya Kwimba Mkoani Mwanza itakayokuwa na wahudumu wa afya ngazi ya jamii 113.
MWISHO
KUPATA PICHA ZAIDI KUHUSU UZINDUZI WA MRADI HUU:-https://simiyuregion.blogspot.com/2018/07/waziri-wa-afya-awataka-waganga-wakuu_13.html
Bariadi - Somanda
Anuani ya Posta: S. L. P. 4, BARIADI.
Simu ya Mezani: 028-2700011/2700054
Simu ya Mkononi: 028-2700011/2700054
Barua Pepe: ras@simiyu.go.tz
Hati Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Simiyu.Haki Zote Zimehifadhiwa