Wanufaika wa Mradi wa Mpango wa Kunusuru kaya maskini TASAF III hususani wanaopewa ruzuku ya utimizaji wa masharti ya elimu na afya wamehimizwa kuwapeleka watoto kliniki na kuhakikisha watoto wao wanahudhuria shuleni.
Wito huo umetolewa na Mkurugenzi wa Ukaguzi wa Ndani kutoka TASAF Makao Makuu, Ndg. Christopher Sanga katika kijiji cha Migato wilayani Itilima wakati wa ziara ya tathmini ya utekelezaji mradi wa TASAF wilayani humo.
Sanga amesema Serikali ina mpango mzuri kwa wananchi wa kuhakikisha watoto wote wenye umri wa kwenda shule wanapelekwa shule na pia watoto wote wenye umri chini ya miaka mitano wanapelekwa kiliniki na kupata huduma za afya zinazotakiwa, hivyo akawaasa kutorudisha nyuma juhudi za Serikali.
Aidha, amesema lengo kuu la Serikali ni kuhakikisha nguvu kazi inajengwa kwa kutoa elimu na kuangalia afya za watoto wakiwa bado wadogo ili watakapobainika kuwa na matatizo ya kiafya wapatiwe matibabu mapema kwa lengo la kuimarisha afya na kutoathiri ukuaji wao.
Ameongeza kuwa utafiti uliofanyika kuhusu utekelezaji wa awamu zilizotangulia za Mpango wa TASAF ulionesha kuwa, kumekuwa na miundombinu mingi ya elimu na afya lakini kaya maskini zimekuwa hazipeleki watoto katika huduma hizo, hivyo Serikali ikatoa ruzuku ya elimu na afya na kuwawekea masharti wazazi ili kuhakikisha wanawapeleka watoto katika huduma hizo.
Amesisitiza kuwa Mpango wa TASAF unafuatilia mahudhurio ya watoto wanaopata ruzuku ya utimizaji wa masharti ya elimu na ili ruzuku hiyo iendelee kutolewa kwa wanafunzi hao ni lazima mahudhurio yao yasiwe chini ya asilimia 80 kwa muhula, wasipohudhuria kuna adhabu inayotolewa ikiwa ni pamoja na kupunguzwa kwa ruzuku hiyo.
“ Miongoni mwa madhara ya watoto kutohudhuria masomo katika muhula husika kwa kaya zinazonufaika na TASAF kwa kupata ruzuku ya elimu ambayo inasaidia kaya hizo, ni kupungua kwa ruzuku na inapopungua uwezo wa kaya katika kujikimu na kufanya mabadiliko ya kiuchumi unaathirika” amesema Sanga.
Kwa upande wake Bibi. Ngolo Buzenganwa mkazi wa kijiji cha Migato ambaye ni mnufaika wa Mpango wa TASAF III amewataka wazazi wenzake kufuatilia maendeleo ya watoto wao na kukagua daftari zao mara kwa mara ili ruzuku inayotolewa isipunguzwe na iwasaidie kuwawezesha kupata mahitaji muhimu ya shule kwa ajili ya watoto wao.
Katika hatua nyingine wanufaika wa Mpango wa TASAF III wameshukuru mpango huo kwa kutatua changamoto ya upungufu wa maji kwa kuwachimbia visima vya maji kupitia programu ya kazi za ajira za muda na kuomba kuongezewa idadi ya visima hivyo katika awamu nyingine ya utekelezaji wa mradi.
“Tunaishukuru sana TASAF kutuletea maji kwa visima hivi, tulikuwa tunatembea muda mrefu sana zaidi ya saa moja kufuata maji, lakini sasa hivi maji yapo karibu tena ni maji safi na salama” amesema Maila Limbu mkazi wa Migato.
Naye Mhandisi wa Maji wa Halmashauri ya Wilaya ya Itilima,Goodluck Masige amesema Serikali Wilayani humo imeweka mpango wa kuviwekea pampu visima vyote 194 vilivyochimbwa kupitia mradi wa TASAF ili kuwarahisishia wananchi kupata maji kwa urahisi zaidi kuliko teknojia inayotuika sasa ya kuvuta kwa kamba.
Wilaya Itilima ni moja ya Wilaya tano zinazofanyiwa tathmini ya utekelezaji wa Mpango wa Kunusuru kaya Maskini (TASAF III) katika awamu hii, tathmini inayofanywa na wataalam kutoka TASAF Makao Makuu, Benki ya Dunia na wadau wengine wa maendeleo (wadau washiriki wa mradi) ambao ni UNDP, UNFPA, ILO pamoja na Umoja wa Nchi za Ulaya(EU).
Bariadi - Somanda
Anuani ya Posta: S. L. P. 4, BARIADI.
Simu ya Mezani: 028-2700011/2700054
Simu ya Mkononi: 028-2700011/2700054
Barua Pepe: ras@simiyu.go.tz
Hati Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Simiyu.Haki Zote Zimehifadhiwa