Wananchi na viongozi kutoka katika vijiji saba vinavyounda Jumuiya ya Hifadhi ya Wanyamapori (WMA) ya Makao hususani Kijiji cha Makao wilayani Meatu Mkoani Simiyu, wamekiri kuwa uhusiano kati yao na Mwekezaji MWIBA HOLDINGS LTD, ambaye amewekeza katika Hifadhi ya Wanyamapori ya MWIBA katika Kijiji cha Makao kwa ajili ya kuendeleza uhifadhi na uwindaji wa kitalii umeimarika tofauti na awali.
Hayo yalibainishwa na wananchi hao jana wakati wa ziara ya Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Simiyu ikiongozwa na Mkuu wa Mkoa huo Mhe.Anthony Mtaka na Kamati ya Siasa ya CCM Mkoa wa Simiyu, iliyoongozwa na Mwenyekiti wa CCM Mkoa Enock Yakobo katika baadhi ya miradi na maeneo ya uwekezaji ya mwekezaji MWIBA HOLDINGS LTD katika Hifadhi ya Wanyamapori ya MWIBA Kijiji cha Makao.
Wamesema awali kulikuwa na mgogoro ambao ulisababisha uhusiano kati wananchi na mwekezaji kuvunjika, lakini baadaye Serikali ya Wilaya na Mkoa ziliingilia kati changamoto zote zilijadiliwa na mapungufu yote yaliyobainika yakafanyiwa kazi, ili pande zote ziweze kunufaika na uwekezaji huo.
“ Uhusiano kati ya Mwekezaji MWIBA HOLDINGS LTD sasa hivi uko vizuri, migogoro iliyokuwepo haipo tena, sasa hivi tunaendelea kuelimishana sisi kwa sisi, ili tusiingize mifugo kwenye eneo lilohifadhiwa kwa utalii maana linatusaidia na tunaendelea kuhamasishana kupambana na ujangili” alisema Andrea Yakobo Mkazi wa Kijiji cha Makao wilayani Meatu.
“Uhusiano uko vizuri, zamani wakati kuna mgogoro tulikuwa tunashuhudia mizoga ya tembo lakini sasa hivi baada ya mwekezaji kushirikiana na wananchi kila mmoja wetu amekuwa mlinzi wa wanyama walio kwenye Hifadhi ya Wanyamapori ya MWIBA, ajira watoto wetu wanapata kama tulivyokubaliana, wantusaidie kwenye elimu, afya na mengine” alisema Amosi Sitta kutoka Kijiji cha Makao.
Mwenyekiti wa Kijiji cha Makao ambaye pia ni Diwani wa Kata ya Mwangudo, Mhe. Anthony Philipo amesema kijiji cha Makao kimenufaika sana kutokana na uwepo wa mwekezaji huyo, hivyo ni vema masuala yote yanayoashiria kuleta migogoro yakadhibitiwa ili wananchi waweze kunufaika na uwekezaji huo.
Naye Mzee maarufu kutoka Kijiji cha makao Bw. Lucas Malyalya amesema pamoja na uhusiano kati ya mwekezaji na wananchi kuwa mzuri wananchi wanaomba suala la mgogoro wa mpaka katika yaWilaya ya Meatu na Wilaya yaNgorongoro(Arusha) katika Kijiji cha Makao lifanyiwe kazi, jambo ambalo liliahidiwa kufanyiwa kazi na Serikali.
Naye Afisa Uhusiano wa MWIBA Holdings Ltd, Bw. Alfred Mwakivike amesema Kampuni hiyo itaendelea kufanya mambo yanayogusa maendeleo ya jamii ikiwemo afya na elimu ambapo amebainisha kuwa kuanzia mwaka huu wameanza kuwasaidia watoto wenye vichwa vikubwa kupatiwa matibabu katika Hospitali ya Sereani iliyoko jijini Arusha.
Aidha, amesema wameanza kuunda vikundi vya vijana kutoka katika Vijini vinavyoizungua Jumuiya ya Hifadhi ya Wanyamapori ya Makao na Rachi ya MWIBA na kuvisajili kwa ajili ya kuwaanzishia miradi ya kuwaingizia kipato ili wasijiingize katika vitendo vya ujangili, badala yake wafikirie pia kuhamasishana ili kuunda vikundi vinavotekeleza miradi itakayosaidia uhifadhi.
Mkurugenzi wa MWIBA HOLDINGS LTD Bw. Abdulkadiri Mohamed ameushukuru uongozi wa Mkoa wa Simiyu kwa kusaidia kumaliza mgogoro kati ya mwekezaji na wananchi na akaomba pia uweze kushirikiana nao katika kutokomeza ujangili na kumaliza suala la mgogoro wa Ardhi na Wilaya ya Ngorongoro ili waweze kufikia lengo la kuendeleza utalii na uhifadhi kama walivyokusudia,
Akizungumza na askari wa kikosi cha kuzuia ujangili cha MWIBA HOLDINGS LTD Mkuu wa Mkoa wa Simiyu,Mhe.Anthony Mtaka amewaka askari hao kufanya kazi zao kwa weledi, kuzingatia sheriana taratibu na kuepuka vitendo vyovyote vya unyanyasaji wa wananchi.
Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Simiyu, Mhe. Enock Yakobo aliwataka MWIBA HOLDINGS LTD kuajiri watumishi waadilifu pia akawaomba viongozi wote wahamasishe na kutoa elimu kwa wananchi kufuata sheria na taratibu ikiwa ni pamoja na kutoingiza mifugo katika eneo la Hifadhi ya Wanyamapori ya MWIBA
MWISHO
KUPATA PICHA ZAIDI KUHUSU TUKIO HILI FUNGUA KIUNGANISHI HIKI:-https://simiyuregion.blogspot.com/2018/07/wananchi-wanaozunguka-hifadhi-ya.html
Bariadi - Somanda
Anuani ya Posta: S. L. P. 4, BARIADI.
Simu ya Mezani: 028-2700011/2700054
Simu ya Mkononi: 028-2700011/2700054
Barua Pepe: ras@simiyu.go.tz
Hati Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Simiyu.Haki Zote Zimehifadhiwa