Mkurugenzi Bodi ya Pamba nchini, Bw. Marco Mtunga amesema Mkoa wa Simiyu utapokea chupa milioni tatu za viuadudu lengo likiwa kukabiliana na changamoto ya wadudu waharibifu wa zao la hilo.
Mtunga ameyasema hayo wakati wa ziara ya Naibu Waziri wa Kilimo, Mhe.Omari Mgumba mkoani Simiyu Machi 06, 2019 ambapo amebainisha kuwa tayari bodi imeshasambaza chupa milioni moja na laki tatu za viuadudu hivyo kwa mkoa huu na kuongeza Simiyu pekee itapokea chupa milioni tatu za viuadudu kwa msimu huu.
“Mpaka sasa chupa milioni moja zimeshafika Mwanza kwa ajili ya Mkoa wa Simiyu kila wilaya itapata chupa laki mbili, awali tulishagawa chupa milioni moja na laki tatu; kutokana na pamba iliyomwa kwa wingi Simiyu lengo letu ni kuipa Simiyu chupa milioni tatu kati ya chupa milioni nane tutakazosambaza nchini msimu huu” alisema Mtunga
Aidha, Mtunga amesema Mkoa wa Simiyu uko katika nafasi ya kuongeza uzalishaji wa zao hilo la pamba kutoka kilo milioni 113 za msimu uliopita mpaka kufikia kilo zaidi ya 300 msimu huu, kutokana na pamba ilivyolimwa kitaalamu na uwepo wa idadi ya miche inayotakiwa kwa ekari.
Akiwa ziarani mkoani hapa Naibu Waziri wa Kilimo, Mhe.Omary Mgumba amesema suala la mbegu za pamba limeenda vizuri hivyo ni vema likaenda sambamba na usambazaji wa viuadudu na kuongeza kuwa wakulima wa zao hilo wameongezeka kutokana na zao hilo kufanya vizuri hususani mkoa wa Simiyu ambao umeongoza kwa uzalishaji ikilinganishwa na mikoa mingine inayolima pamba hapa nchini.
“Suala la mbegu lilienda vizuri lakini kubwa zaidi ni mahitaji makubwa kuliko matarajio kutokana na hamasa mliyofanya mwaka jana watu wengi walihamasika kulima pamba, hata mwaka huu wengi zaidi watakuwa wamelima, maana wakulima wengi huwa wanahamasika kulima zao ambalo limefanya vizuri msimu uliopita” alisema Mgumba.
Awali akimkaribisha Naibu Waziri wa Kilimo, Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka amesema kuwa lengo la mkoa ni kuongeza uzalishaji kwa ekari kuanzia kilo 500 hadi 1000 kwa ekari badala ya kuongeza idadi ya wakulima pekee.
“Tungehitaji kuongeza uzalishaji kwa ekari badala ya kuongeza uzalishaji kwenye idadi ya wakulima, mwaka 2018 tulivuna kilo milioni 113, mwaka huu uzalishaji utaongeza lakini unaweza kuongezeka kutokana na ongezeko la wakulima na ekari zilizolimwa; wakati tunaweza kupata kilo kama hizo kwenye pungufu ya ekari na idadi ya wakulima kama tutaongeza uzalishaji kwa ekari”
“Msukumo wa Mkoa ni kuona tunaongeza uzalishaji kwa ekari, ukienda Mwabusalu kuna wakulima wanazalisha kuanzia kilo 500 hadi 1000 kwa ekari , kwa hiyo kama mkoa tumejipanga kuhakikisha uzalishaji unaongezeka kwa ekari na idadi ya wakulima pia inaongeza” alisema Mtaka.
Naibu Mgumba yuko mkoani Simiyu katika ziara ya kikazi yenye lengo la kukagua shughuli za kilimo na ushirika zinavyoendelea pamoja, kukagua shughuli za miradi ya umwagiliaji akiwa Wilayani Itilima amepata nafasi ya kuzugumza na wananchi kupitia mkutano wa hadhara.
MWISHO
KUPATA PICHA ZAIDI KATIKA HABARI HII FUNGUA KIUNGANSHI HIKI:-https://simiyuregion.blogspot.com/2019/03/simiyu-kupata-chupa-milioni-tatu-za-wa.html
Bariadi - Somanda
Anuani ya Posta: S. L. P. 4, BARIADI.
Simu ya Mezani: 028-2700011/2700054
Simu ya Mkononi: 028-2700011/2700054
Barua Pepe: ras@simiyu.go.tz
Hati Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Simiyu.Haki Zote Zimehifadhiwa