Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.Anthony Mtaka amesema Maonesho ya Sikukuu ya Wakulima (Nanenane) yalenge kuwashindanisha washiriki katika vigezo vinavyolenga kutatua tatizo la njaa na kuwainua wananchi kiuchumi badala ya kuwashindanisha kwa ujenzi wa mabanda.
Mtaka ameyasema hayo wakati akihitimisha maonesho ya Nanenane Kanda ya Ziwa yaliyofanyika katika Uwanja wa Nyamhongolo wilaya ya Ilemela Jijini Mwanza.
Amesema Halmashauri zimekuwa zikishindanishwa na kupata tuzo na vyeti kwa kuwa na mabanda mazuri , kutembelewa na watu wengi na vigezo vingine vinavyowekwa kutathmini wakati wa maonesho, lakini wananchi katika baadhi ya maeneo hayo wanapata tatizo la njaa.
Ameongeza kuwa ipo haja kwa viongozi wa mikoa ya Kanda ya Ziwa ambayo ina uhakika wa maji ya Ziwa Victoria kuweka dhamira ya kuondokana na aibu ya kuomba chakula cha msaada ili kuisaidia Serikali.
“ Ni vizuri tujiulize sana sisi viongozi wa Kanda ya Ziwa tunaokuja kwenye maonesho ya Nanenane; ni kwa nini Mhe.Rais asiombwe chakula maeneo yasiyo na maji ya uhakika, aombwe chakula na watu wenye maji ya uhakika, ipo haja ya kuweka dhamira ya dhati kuondokana na aibu hii” alisema Mtaka.
Aidha Mtaka amesema ili kufanya mapinduzi katika kilimo Wataalam wa Kilimo wanapaswa kuwasaidia wakulima kuondokana na kilimo cha mazoea ili waweze kulima kilimo cha kisasa chenye tija.
Sanjali na hilo Mtaka ametoa wito kwa Benki ya Maendeleo ya Kilimo kuwasaidia wananchi kupata mbegu bora, mbolea na zana bora za kilimo yakiwemo matrekta ili waweze kutoka kwenye kilimo cha utamaduni(mazoea) kwenda kwenye kilimo cha kisasa chenye tija.
Mkuu huyo wa Mkoa pia ametoa rai kwa Wataalam wa Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kutoka Maofisini na kuwasaidia wakulima, wafugaji na wavuvi kupata elimu ya ugani ili wafanye shughuli zao kwa tija na weledi.
“Watu wa Wizara tokeni huko wizarani njooni muwafundishe watu wetu ugani...tunakwazwa sana na ninyi watu wa Wizara hasa mnapoona ni jambo jepesi kutoa maagizo kwa wakuu wa wilaya wasimamie Kilimo wakati ninyi mnajua mnaleta mbegu zisizo na kiwango,madawa mnayoleta yana changamoto ya kuwa feki” amesema Mtaka.
Ameongeza kuwa Viongozi wa kanda ya ziwa wanaomba Wizara ya Kilimo kuja na majawabu ya kudumu ya changamoto za uzalishaji wa zao la pamba hususani upatikanaji wa mbegu bora, madawa pamoja na bei ya kuuzia pamba itakayowasaidia wakulima wa pamba.
Katika hatua nyingine Mwenyekiti wa Tathmini ya Maonesho ya Nanenane, Mathayo Masele aliitangaza Halmashauri ya Wilaya ya Busega kutoka Simiyu kuwa Halmashauri ya kwanza kati ya Halmashauri za Mikoa yote ya Kanda ya Ziwa kwa kutimiza vigezo vilivyotumika kushindanisha ikiwa ni pamoja na utekelezaji wa Kauli Mbiu ya maonesho.
Akizungumzia ushindi huo Mkuu wa Idara ya Kilimo, Umwagiliaji na Ushirika Wilaya ya Busega, Ndg.Juma Chacha amesema Halmashauri hiyo ilitimiza vigezo vyote vya ushindani kwa asilimia 100 , ambapo ilikuwa na vitalu vya mfano kwa mazao ya chakula na biashara,mabanda ya mifugo mbalimbali, ufugaji wa samaki kwa ajili ya elimu kwa wakulima, wafugaji na wavuvi namna ya kuongeza thamani.
Naye Emmanuel Mgeta mkulima kutoka Busega aliyekuwa mshindi wa tatu kati ya wakulima wa mikoa ya kanda ya ziwa walioshindanishwa amesema maonesho ya Nanenane mwaka 2017 yamemsaidia kujifunza na kumpa hamasa ya kufanya vizuri katika uzalishaji na umuhimu wa kuyaongezea thamani mazao.
Kauli Mbiu ya Nane nane mwaka 2017 ni “ZALISHA KWA TIJA MAZAO YA KILIMO,MIFUGO NA UVUVI ILI KUFIKIA UCHUMI WA KATI” ambapo Mikoa ya Kanda ya Ziwa Simiyu, Mwanza, Geita, Mara, Shinyanga na Kagera imeadhimisha katika Uwanja wa Nyamhongo Ilemela jijini Mwanza.
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka akimkabidhi Mkuu wa Idara ya Kilimo, Umwagiliaji na Ushirika Halmashauri ya wilaya ya Busega,Juma Chacha zawadi ya kombe na cheti baada ya Halmashauri hiyo kushika nafasi ya kwanza miongoni mwa Halmashauri za Mikoa ya kanda ya Ziwa katika Maonesho ya Nanenane Kanda ya Ziwa katika Uwanja wa Nyamhongolo Ilemela Jijini Mwanza.
Katibu Tawala Mkoa wa Simiyu, Ndg.Jumanne Sagini (katikati) akipata maelezo kutoka kwa watalaam wa Kilimo kuhusu zao la dengu mara baada ya kutembelea Banda la Halmashauri ya Wilaya ya Busega na kuona vitalu vya baadhi ya mazao ya Kilimo na biashara, kwenye Maonesho ya Nanenane Kanda ya Ziwa katika Uwanja wa Nyamhongolo Ilemela Jijini Mwanza.
Bariadi - Somanda
Anuani ya Posta: S. L. P. 4, BARIADI.
Simu ya Mezani: 028-2700011/2700054
Simu ya Mkononi: 028-2700011/2700054
Barua Pepe: ras@simiyu.go.tz
Hati Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Simiyu.Haki Zote Zimehifadhiwa