Katibu Tawala wa Mkoa wa Simiyu, Bi. Miriam Mmbaga leo amefanya kikao na Uongozi wa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii NSSF na baadhi ya waajiri wa sekta binafsi mkoani Simiyu kwa lengo la kujadili ulipaji wa madeni ya michango ya waajiriwa NSSF, ambapo katika kikao hicho imeazimiwa kuwa waajiri wote wa sekta binafsi wanaodaiwa wahakikishe wanalipa madeni hayo kwa wakati.
Akizungumza na waajiri wa sekta binafsi katika kikao hicho Bi Mmbaga amesema suala malipo ya michango ya mfuko wa hifadhi ya jamii ni suala la kisheria na lina manufaa kwa pande zote mbili (waajiri na waajiriwa), hivyo ni vema NSSF iendelee kutoa elimu ili kila upande ujue na utimize wajibu wake.
“Jambo hili lipo kisheria na lina faida kwa pande zote mbili mwajiri na mwajiriwa, kwa mwajiri kwamba hatasumbuliwa kwamba amekiuka sheria lakini mwajiriwa akiwa mwajiri anayelipiwa michango yake ya pensheni atatambua kuwa mwajiri wake anajali maslahi yake,”alisema Mmbaga.
Aidha, Mmbaga amesema azimio jingine la kikao hicho ni Mfuko wa hifadhi ya jamii NSSF Mkoa wa Simiyu kuhakikisha kuwa unatoa vitambulisho vya waajiriwa ambao waajiri wao wametimiza masharti ya kuanza kuwalipia michango ya mfuko wa hifadhi ya jamii mpaka kufikia Septemba 10, 2020 .
Wakati huo huo Mmbaga amesema Mkoa utaendelea kufanya vikao na wadau angalau mara tatu kwa mwaka kwa lengo la kuelimieshana na kujadiliana masuala mbalimbali ikiwemo namna sahihi ya utatuzi wa changamoto mbalimbali ili waweze wadau waweze kufanya kazi zao kwa tija na kuendana na dira ya mkoa yenye lengo la kuwa mkoa shindani kiuchumi.
Kwa upande wake Kaimu Meneja wa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii NSSF, Bw. Nuru Mmbaga amesema ni wajibu wa kila mwajiri katika sekta binafsi kulipa michango ya mfuko wa hifadhi ya jamii kwa kutoa asilimia 10 ya mshahara ghafi wa mwajiriwa nay eye mwajiri kulipia asilimia 10 pia kwa mujibu wa sheria.
Naye Mwanasheria wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Bi. Mwanahamisi Kawega amesisitiza umuhimu wa waajiri kulipa madeni ya michango ya waajiriwa wao kwa mfuko wa hifadhi ya jamii NSSF ili waajiri wao waweze kupata haki na stahili zao mathalani mafao ya uzazi.
Kwa upande wao waajiri wa sekta binafsi walioshiriki katika kikao hicho wameshukuru uongozi wa Mkoa kuitisha kikao hicho ambapo wamekiri kuwa wako tayari kulipa madeni yote halali ya michango ya waajiriwa wao huku wakisisitiza elimu iendelee kutolewa kwa waajiri na waajiriwa ili wawe na uelewa wa pamoja kuhusu haki na wajibu wao katika masuala ya hifadhi ya jamii.
“Tunashukuru kwa kikao kizuri ambacho umekuwa na mjadala mzuri, sisi tuko tayari kulima madeni hayoa lakini kinachotakiwa ni NSSF kutusaidia kutoa namba za utambulisho maana watumishi wetu wengi walikataa fedha zao kukatwa kutokana na kutokuwa na namba, tunaombba namba zitolewe kwa wakati,” alisema Bi.Tina Chenge Mkurugenzi wa Madina Bakery Company.
“Tunaomba elimu kwetu na kwa watu wetu iendelee kutolewa maana tunafanya kazi tofauti na tunaajiri watu kwa namna tofauti mfano katika viwanda kuna waajiriwa tunakuwa nao kwa miezi miwili au mitatu, nashauri tukae chini tuangale madeni yote halali tulipe na NSSF itoe kadi za utambulisho kwa waajiriwa wetu ambao tuanze kuwalipia michango yao mara moja,” alisema Gungu Silanga Mkurugenzi kampuni ya Nsagali.
MWISHO
KUPATA PICHA ZAIDI FUNGUA KIUNGANISHI HIKI:-https://simiyuregion.blogspot.com/2020/09/ras-simiyu-awataka-waajiri-sekta.html
Bariadi - Somanda
Anuani ya Posta: S. L. P. 4, BARIADI.
Simu ya Mezani: 028-2700011/2700054
Simu ya Mkononi: 028-2700011/2700054
Barua Pepe: ras@simiyu.go.tz
Hati Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Simiyu.Haki Zote Zimehifadhiwa